Ilemela shida ya maji itakuwa historia - DC Masalla


Mkuu wa wilaya ya Ilemela Mhe Hassan Elias Masalla amesema kuwa shida ya Maji ndani ya wilaya hiyo itakuwa historia baada ya kukamilika kwa miradi mikubwa inayotekelezwa wilayani humo ukiwemo ule wa ujenzi wa Tanki la Maji la mlima wa Kwa Mkuu wa wilaya kata ya Buswelu uliogharimu zaidi ya shilingi bilioni Tano.

Hayo ameyabainisha wakati wa muendelezo wa ziara yake ya kata Kwa kata kukagua utekelezaji wa shughuli za maendeleo, kuhamasisha wananchi kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa wa UVIKO-19 na kujitokeza kwaajili ya chanjo pindi zitakapowasili wilayani humo, kusikiliza kero na changamoto za wananchi na kisha kuzipatia ufumbuzi akiwa ameambatana na wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama, wakuu wa idara za manispaa ya Ilemela, wataalamu wa taasisi za TARULA, TANROADS, TANESCO, NIDA na RITA ambapo akawahakikishia wananchi wa kata ya Mecco waliojitokeza katika viwanja vya Jerry’s kumsikiliza, Kuwa anatambua wilaya hiyo kukabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa Maji ya uhakika hasa maeneo ya milimani na yenye sura ya vijiji kwamba Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Mhe Samia Suluhu Hassan imekwisha toa fedha kwaajili ya ujenzi wa mradi huo mkubwa wa Maji na kwamba Mbio Maalum za Mwenge wa Uhuru Kwa mwaka huu zimeweka jiwe la msingi na Mapema mwezi septemba mradi huo utakuwa umekamilika


‘.. Kufikia mwezi septemba shida ya Maji itakuwa imeisha kama sio kupungua Kwa kiasi kikubwa, Sisi hatuwezi kukaa ofisini kama wananchi hamna Maji ..’ Alisema 

Aidha Mhe Masalla akampongeza Mbunge wa Jimbo la Ilemela Mhe Dkt Angeline Mabula Kwa namna anavyoshiriki katika kushughulikia kero za wananchi huku akilishukuru jeshi la polisi wilayani humo Kwa namna linavyofanya kazi kwa weredi 

Kwa upande wake Mhandisi Josephat Ilunde kutoka mamlaka ya Maji safi na Maji taka jijini Mwanza MWAUWASA akafafanua kuwa Jiji hilo linahitaji Lita milioni 150 za Maji, wakati zilizopo ni Lita milioni 90 hivyo kuwa na upungufu wa Lita milioni 60 ambazo zitapatikana baada ya kukamilika Kwa chanzo Cha Maji Cha Butimba kinachogharimu zaidi ya bilioni 77 na kukamilika kwa miradi mingine inayoendelea ndani ya wilaya ya Ilemela 

Nae kaimu mkurugenzi wa manispaa ya Ilemela Ndugu Shukran Kyando mbali na kuahidi kutekeleza maelekezo yote yaliyotolewa na Mkuu huyo wa wilaya amezitaka mamlaka za kata ya Mecco kuheshimu mipaka ya kata hiyo iliyotangwa mara ya mwisho katika gazeti la Serikali sanjari na kuiagiza kampuni inayofanya kazi ya urasimishaji makazi mtaa wa Mecco Kusini kuhakikisha inawasilisha ramani ndani ya siku 14 zilizotolewa na Mkuu wa wilaya hiyo Kwa wananchi Ili kuwaondolea usumbufu katika Zoezi la umilikishaji na kuikosesha Serikali mapato.

 

Comments